STORY:WAMEGOMBANA, WANATAKA KUACHANA? WE’ INAKUHUSU NINI?



Ni Ijumaa nyingine nzuri tunapokutana tena nawe msomaji wangu, nategemea uko poa kwa kudra za Mungu na unaendelea vizuri na majukumu yako ya kila siku. Karibu kwenye uwanja wetu huu na leo nataka kuzungumza nawe mada ya tofauti kidogo.

Jambo lenyewe ninalotaka kuzungumza nawe msomaji wangu, ni tabia waliyonayo baadhi ya watu ya kushadadia matatizo ya kimapenzi yanayotokea kwenye maisha ya watu wao wa karibu, wawe ndugu, marafiki, majirani au watu ambao wanachangamana nao kwa namna moja au nyingine.
Yaani mtu wako wa karibu amekorofishana na mwenzi wake, wewe badala ya kutoa ushauri mzuri au kunyamaza kimya kama huna ushauri wa kujenga, matokeo yake unashadadia na kuendelea kumwaga sumu ili ugomvi uzidi kuwa mkubwa au waachane kabisa.

Bila shaka msomaji wangu utakuwa umeshakutana na watu wa aina hii ambao wao kazi yao kubwa ni kushangilia matatizo ya wenzao au yawezekana wewe pia ni miongoni mwa watu wa aina hiyo.
Siri kubwa ambayo huijui, wahenga wanasema ndugu wakigombana chukua jembe ukalime. Watu wanaopendana kwa dhati, ambao wameshaishi pamoja au wana ndoto za kuja kuishi pamoja, wanakuwa sawa na ndugu.

Inapotokea wakagombana, kuwa makini sana usishadadie matatizo yao. Kama una busara, simama katikati kujaribu kuwashauri wamalize tofauti zao ili maisha yaendelee.
Lakini kama kazi yako ni kuchochea kuni, kuongeza chumvi na kutoa ushuhuda wa uongo ili tu wazidi kugombana na mwisho waachane, elewa kwamba mwisho wake utaadhirika.

Mapenzi ya kweli huwa hayafi kirahisi hata kama yamekumbwa na kimbunga kikubwa kiasi gani. Hujawahi kuona mume amezaa nje, mke amejua na ugomvi mkubwa umetokea kiasi cha kufikia hatua ya kutaka kutengana lakini mwisho wanayamaliza na maisha yanaendelea, tena kwa upendo kuliko mwanzo?

Hujawahi kuona wenza wanakoseana makosa makubwa-makubwa, wanapigana na kudhalilishana kiasi kwamba kila mtu anajua wamefika mwisho lakini baada ya kila mmoja kukaa na kutulia, wanarekebisha kasoro na maisha yanaendelea, tena kwa mahaba mazito kuliko mwanzo?

Nakupa mifano hii ili uelewe kwamba nguvu ya mapenzi ya kweli ni kubwa sana. Linaweza kutokea tatizo kwa wanandoa au wenzi ambao unawajua, ukajiaminisha kwamba hawawezi kurudiana tena, ukachochea kuni na kuongeza chumvi kadiri uwezavyo lakini mwisho ukawaona wako pamoja tena, mahaba yakiwa yamekolea kuliko mwanzo.

Wakishapatana, wataambizana yale yote uliyokuwa unayasema, kila mmoja atamueleza ukweli mwenzake juu ya nani na nani walikuwa wanashadadia waachane. Hujanunua ugomvi na chuki kali mpaka hapo?
Kama wewe ni mtu unayejiheshimu, mwenye busara na usiyetaka matatizo na binadamu wenzako, unapaswa kujizuia sana kushadadia matatizo ya kimapenzi yanayowatokea watu wako wa karibu.
Hata kama mmoja kati yao amekufuata kuomba ushauri, jitahidi sana ushauri wako uwe ni wa kujenga na kumaliza tofauti kati yao. Usimshauri mtu aachane na mwenzi wake kwani mwisho wa siku, uamuzi unabaki kwake mwenyewe.

Ni makosa sana kuanza kumhadithia mabaya ya mwenzi wake mtu ambaye yupo kwenye matatizo. Kauli mbaya kama za ‘huyo ameshindikana, watu kibao wamepita hapo utakuwa wewe?’, ‘yule mwanamke malaya sana, hakufai’ au ‘huyo siyo mume, anakupotezea muda wako tu’ ni sumu kali ambayo unapaswa kuizuia isitoke kupitia kinywa chako.

Walipokutana hukuwepo, umeanza kuwaona tu wakiwa pamoja kwa hiyo maisha yao hayakuhusu. Badala ya kupoteza muda wako kukoleza makaa kwenye penzi lao linaloyumbayumba, ni vyema ukaelekeza nguvu kulinda penzi lako ili na wewe yasije kukukuta kama yanayowatokea wenzako.

Kwa leo niishie hapa, kwa ushauri, maoni nicheki kwa namba za hapo juu. Tukutane wiki ijayo kwa mada nyingine nzuri.

LOVE STORY:UNAMPENDA, UNATAKA NDOA

 
Ni wiki nyingine ambapo Mwenyezi Mungu ametujaalia kukutana katika busati letu la mahaba kujadiliana mambo mbalimbali yanayohusu uhusiano wa kimapenzi. Ni matumaini yangu kuwa mada ya wiki iliyopita ilikuingia vizuri na sasa unayafanyia kazi yale tuliyojadiliana.

Karibu tena tujadiliane kuhusu mada ya leo kama inavyojieleza; unampenda na unataka kumuoa lakini hujui pa kuanzia, unapaswa kufanya nini?

Maendeleo ya teknolojia yamebadilisha mambo mengi katika maisha yetu ya kila siku. Zamani ilikuwa kama kuna mwanamke au mwanaume unampenda, basi lazima uhangaike sana mpaka utakapopata nafasi ya kuzungumza naye, na kama huna ujasiri wa kumtongoza ana kwa ana basi ndiyo umemkosa.
Siku hizi mambo yamebadilika sana. Ukitokea kumpenda mtu fulani kama kweli nia yako ni kuingia naye kwenye ndoa na siyo kukidhi matamanio ya siku moja, zipo mbinu nyingi zinazoweza kukurahishia kazi yako. Kuna simu za mikononi, kuna mitandao ya kijamii na njia chungu nzima hivyo huna haja ya kuendelea kuumia na upweke.

Kumbuka kuwa penzi bora ni lile ambalo wawili huanza kwa kuwa marafiki, ni makosa kukurupuka kumtongoza mtu kwenye simu au kwenye mitandao ya kijamii bila kumvuta kwanza karibu yako na kumfanya kuwa rafiki yako.

Hatua ya kwanza, kama nilivyosema hapo juu ni kujitahidi kujenga ukaribu naye. Kama unadhani ni vigumu kwa wewe na yeye kukutana ana kwa ana, unaweza kutafuta namba yake ya simu. Ukishapata namba ya simu ya huyo umpendaye, tafuta muda ambao utakuwa umetulia kisha mpigie na jitambulishe. 
Mweleze kwamba umempigia simu kumjulia hali, kama akikuuliza mahali ulikoipata namba yake, unaweza kumjibu vyovyote lakini inashauriwa kuwa siyo vizuri kumtajia aliyekupa namba yake kwa sababu unaweza kuwagombanisha.

Usiwe na papara, mtakie siku njema na endelea na shughuli zako nyingine. Unaweza pia kuendelea kumtumia meseji za kawaida (siyo za mapenzi), ukimjulia hali, ukimuuliza kama ameshakula au amekula chakula gani, anafanya nini kwa muda huo na vitu anavyovipenda sambamba na vile asivyovipenda.

Endelea hivyo kwa muda, siri kubwa ambayo huijui ni kwamba watu wengi, hasa wanawake huwa wanapenda kujua kuwa mtu fulani anamjali kwa kumuuliza mambo mbalimbali yanayohusu maisha yake ya kawaida. Jitahidi kuwa mcheshi lakini usizidishe masihara. Ukishafanikiwa kumvuta karibu yako na kumfanya aamini kwamba huwa unamfikiria mara kwa mara, sasa unaweza kupiga hatua moja mbele kwa kufanya yafuatayo:

Tumia sauti ya utulivu yenye hisia ndani yake, utazidi kumvuta karibu yako. Usipende kuzungumza kwa sauti ya juu au kupayuka au kupiga simu ukiwa kwenye kelele. Akipokea tu simu yako, mjulie hali yake kisha msifie kidogo kuhusu sauti yake na namna anavyozungumza.
Msimulie kidogo kuhusu siku yako inavyokwenda, tumia maneno machache lakini yatakayomfanya asiboreke kukusikiliza. Ifanye stori yako iwe ya kuvutia kwa kutumia maneno matamu yatakayomfurahisha na kumfanya aache kila anachokifanya na kukusikiliza.

Badili mazungumzo, muulize kama anajua kwamba yeye ni mzuri sana na hujawahi kukutana na mtu anayevutia kama yeye. Kama wewe ni mwanaume na unayezungumza naye ni mwanamke, utakuwa katika nafasi nzuri ya ‘kum-win’ kwa sababu wanawake wengi wanapenda sana kusifiwa.

Akiwa amekolea na sifa unazommwagia, mweleze kwamba unavutiwa naye na unatamani kuwa na mpenzi anayefanana naye. Zungumza naye kwamba atakapokubali kuwa na wewe, utamtunza na kumlea kama malkia, mweleze malengo yako ya baadaye katika uhusiano wenu endapo atakukubalia.

Usimpe nafasi ya kukwambia kama amekubali au amekataa bali hitimisha mazungumzo yenu kwa kumtakia siku njema au kazi njema. Bila shaka utamuacha akiwa na shauku kubwa ya kuendelea kusikiliza ‘mistari’ yako. 
Endelea kuwasiliana naye kwa mambo ya kawaida huku ukimpima kama yale uliyomwambia anayachukuliaje. Kama naye amekupenda, utaanza kuona mabadiliko kuanzia meseji atakazokuwa anakutumia.

Itaendelea wiki ijayo.
Older Posts
© Copyright VIJIMAMBOZI Published.. Blogger Templates
Back To Top